Translate

Fasihi

Je, fasihi ni nini? 
 Ili kujibu swali hili, ni vyema kurejelea baadhi ya wataalamu ili kupata fasili zao katika kueleza maana ya fasihi. 
 Oriedo, (2007) anasema kuwa fasihi ni:
Taaluma inayoshughulikia kazi za sanaa zinazotumia lugha kisanii.
Wamitila,(2003) anasema kuwa dhana hii ni pana mno ambayo ni vigumu kueleza kwa ufupi. Kulingana naye, ili kufafanua dhana hii ni lazima tutambue kuwa ni 
...kazi za kisanaa...zilizotumia lugha kwa usanii na zinazowasilisha suala fulani pamoja kwa njia inayoathiri, kugusa na kuacha athari fulani na kuonyesha ubunilizi na ubunifu fulani na zinazomhusu binadamu.
Naye Mogambi, (2008) anadokeza vigezo vitatu vya kuzingatia katika kufafanua fasihi:
Utumiaji wa lugha kisanaa; utungaji wa utungo kutokana na taratibu na hali mbalimbali za maisha; ubunifu (uk111)
Kulingana na Bakhressa, (1992) anafafanua fasihi kwa kutolea mifano ya tanzu zake kama vile mashairi, tamthilia 
...na mitungo ya sanaa katika lugha.
Wataalamu wengine ni Kimani Njogu na Rocha Chimera (2008).Hawa wanasema hivi kuhusu dhana hii:
Fasihi...ni chombo chenye misingi yake katika ubunifu...(ni) aina ya sanaa inayotumia lugha ili kuelezea tajiriba za binadamu.
Kutokana na fasili hizi, tunapata mambo matatu makuu yanayoshamiri katika ufafanuzi wa fasihi. Kuwa:
  • Fasihi ni kazi ya sanaa
  • Lugha ndiyo wenzo mkuu katika kuwasilisha fasihi
  • Fasihi huakisi maisha ya binadamu kibunifu
Hivyo basi tunaweza kusema kuwa:
Fasihi ni kazi ya sanaa inayotumia lugha kibunifu ili kuelezea maisha ya binadamu.
 
Hii inaashiria kuwa fasihi ni mojawapo tu ya sanaa kama zilivyo uchoraji, uchongaji, ufinyanzi na ususi. Naam, jinsi mfinzanzi atakavyotumia udongo kuumba sanamu kuashiria mtu hodari kama vile Fumo Liyongo ndivyo mchoraji atakavyotumia picha kumchora. Naye mchongaji atatumia mawe au mbao huku mwandishi/ msimulizi akimchora nguli huyo kwa kutumia maneno (ambayo hujenga lugha). Ili kutoa sifa zote alizopewa babe huyo Liyongo, basi msanii  wa fasihi lazima atumie ubunifu. Ni ubinifu huu utakaomwezesha kumsawiri mhusika kwa uwazi licha ya yeye kumwona katika ulimwengu halisi. 


Marejeleo
Bakhressa, K. S. (1992). Kamusi ya Maana na Matumizi. Oxford University Press. Nairobi: Kenya
Mogambi, H. (2008). K. C. S. E. Golden Tips Kiswahili. Macmilan Publishers. Nairobi: Kenya
Njogu, K. na Chimerah, R.(2008). Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu. Jomo Kenyatta Foundation. Nairobi: Kenya.
Oriedo, E. H. (2007). Istilahi za Fasihi ya Kiswahili. Kenya Literature Bureau. Nairobi: Kenya
Wamitila, K. W. (2003). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Focus Publications Ltd. Nairobi: Kenya.
 









Post a Comment

 
Usaidizi : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2014. Swahili - Haki zote zimehifadhiwa
Imeundwa na Creating Website Ikachapishwa na Mas Template
Imeletwa kwako na Balozihumu