Translate

Mstahiki Meya: Mukhtasari wa Matukio

Saturday, March 29, 20140 comments


Sehemu ya I
I
Daktari Siki yumo Zahanatini. Anaranda huku na huku. Milio ya watoto inasikika kwa mbali. Waridi anaingia na kumwarifu kuwa wagonjwa wamefika wengi kuliko kawaida. Vilevile anamjuza kuwa dawa hazipo japo habari ni kwamba zimo safarini katika bahari kuu. 

Daktari anakata kauli ya kuwashughulikia wagonjwa kwa dawa ziizopo. Ghafla, mama mmoja anaingia na mtoto aliye hali maututi. Mtoto huyo anaendesha baada ya kula maharage yaliyolala kutoka kwa Meya. Siki anamshauri Waridi kumwandalia mchanganyiko wa sukari na chumvi katika maji moto. Baadaye daktari anapendekeza kuwa wagonjwa waliozidiwa walazwe- kauli ambayo Waridi anapinga. (uk7).
II
Onyesho linafanyika nyumbani kwa Meya. Mwenyewe ameketi mezani kwa maakuli. Daktari anafika na kumlalamikia hali duni ya baraza. Anakashifu uongozi duni wa nduguye Sosi. Malumbano kati yao yanaendelea hadi Meya anapomfukuza daktari na kuagiza kuwa asirudi kwake tena.
III
Hapa ni kwenye afisi ya Meya. Madiwani watatu wamefika na kumsubiri. Wao ni:
Diwani I: Kinara wa Masuala ya Usalama
Diwani II: Kinara wa Uhusiano Mwema
Diwani III: Kinara wa Uchumi na kazi
Kabla ya Meya kuingia, watatu hawa wanazungumzia uongozi wa baraza. Diwani I na II wanaelekea kukubaliana ilhali Diwani III anaelekea kujitenga kwa kupinga swala la kuwapa watu ahadi zisizotimizwa.

Meya anaingia na kudai kuwa kuna baadhi ya madiwani ambao wanachochea watu dhidi ya uongozi wa baraza. Anawaulizia kila mmoja hatua wanazotekeleza katika vitengo vyao. Baada ya majibu, kikao kinakamilika kwa maagano.

Sehemu II
I
Tendo hili ni la mwezi mmoja baada ya maonyesho ya sehemu ya kwanza. Meya yumo afisini kuandaa mapokezi ya mameya kutoka nchi za nje. Bili, rafiki yake anasasili. Wanazungumzia familia zao. Hii ni kando na shauri la Bili kuhusu namna ambavyo Meya atashughulikia kesi ya mwanakandarasi mmoja.

Punde sauti inasikika nje. Sauti hiyo inalalamikia haki za wananchi. Wamechoka kudhalilishwa. Bili anmwambia Meya kuwa asihofu kwani

...wasemao mchana usiku watalala...(uk31).
Gedi anaingia na habari za watu kugoma. Anrudishwa nje na Meya kwa kuwatahadharisha wanaogoma. Kidogo tena Gedi anarejea tena na taarifa kuwa wanahabari wangependa kumhoji Meya. Meya anadinda kutoka nje kwa madai kuwa yu mkutanoni. Baadaye wanaagana kwa ahadi kuwa Bili atampitia Mhubiri kumweleza hitaji la maombi kwa Meya.
II
Onyesho limo afisini mwa Daktari Siki. Anapokea simu na baadaye kuanza kujizungumzia. Waridi anaingia kwa kasi. Anadai kuwa ameamua kujiuzulu. Sababu anayotoa ni kuwa watu wanafia mkononi mwake kwa ukosefu wa dawa. Tatu anaingia na kukatiza mazungumzo baina yao. Waridi anaondoka. Tatu, mwakilishi wa wafanyakazi, anamtaka Siki ampelekee Meya malalamishi ya wafanyakazi. Daktari anasema kuwa hilo haliwezekani ila wao wafanyakazi wazidi kususia.


III

Onyesho linafanyika afisini mwa Meya.  Mhubiri ameitikia mwito wa kuja kumwona na kumwombea Mstahiki. anapongezwa kwa kutii wito huo. Mhubiri anaposema kuwa i wajibu wake kuitika anapoitwa, Meya anadai kuwa huwa anahisi kumfuata mhubiri katika imani. Baadaye wanaanza maombi ambayo yanaishia kwa kelele. Ni kelele hizi zinazowapelekea Gedi na askari kudhani kuwa Meya amevamiwa. Wao wanakuja mbio na kuwaamrisha Meya na Mhubri kulala chini ili wajisalimishe. Wanapogundua kuwa hakuna fujo na kuwa wamekosea kumwamrisha Meya, Gedi anajitetea kwa kusema hivi;
...tulisikia kelele tukadhani vinyangarika wameleta fitina zao humu. (uk43).
Baadaye Meya anawaruhusu kuondoka. Mhubiri anaendelea kumhimiza mwenyeji wake kwa kudai kuwa mateso aliyopata Bwana hayalinganishwi na tendo hili la akina Gedi.

Mstahiki Meya anatoa ombi kuwa mhubiri awe akifika afisini mara moja kwa wiki kuliombea baraza. Anaahidi kuwa gharama ya petroli itashughulikiwa na baraza hilo. Aidha, litatoa sadaka ya shilingi laki moja kila mwezi kama njia moja ya kutambua umuhimu wa dini. Onyesho linaisha wawili hao wakipokezana mikono.
IV
  Nyumbani kwa Diwani Kheri. Siki na Diwani III wameketi barazani. Wanajadili hali kama ilivyo barazani.  Dkt. Siki amekuja kumsihi Kheri kuzungumza na Meya ili ashughulikie maslahi ya wananchi. Katika maongezi yao tunapata yafuatayo:
  • Japo Siki ni binamuye Meya, hawapatani abadani.
  • Katika baraza kuna mgawanyiko uongozini (uk 47)
  • Vimo vipengele katika sheria vinavyompelekea kiongozi kutenda maovu bila kuzuiwa. Hivi ni pamoja naMayor's act, Riot act na Collective responsibility.
  • Wananchi ndio waliowachagua viongozi hao wanaolalamikia.
  • Kuna mianya katika baraza inayochangia ufisadi kukithiri
 Diwani anamruhusu Siki kuondoka.

Sehemu III

I
Onyesho linafanyika afisini mwa Meya. Mwito wa Meya kwa Diwani unasadifu na azma ya diwani huyo kutaka kumwona. Kunazuka majadiliano makali baina yao. Meya anamtaka Diwani III kuongeza mishahara ya madiwani. Hili linapingwa vikali na Diwani III kwani baraza haliwezi kumudu mishahara hiyo licha ya kilio cha mishahara duni ya wafanyakazi wengine. Meya anamshurutisha kutekeleza amri yake pasi kujali maslahi ya wananchi wa kawaida. Diwani anakubali kutekeleza wajibu huo shingo upande. Anaondoka na kumwacha Meya peke akiwaza.
II
Onyesho hili linakita katika afisi ya Mstahiki Meya. Sauti za wafanyakazi wakilalamikia haki zao zinasikika. Meya anatazama dirishani na kisha kuanza kusoma gazeti. Sauti ya kiongozi wa wafanyakazi inasikika akiwasihi wenzake kuungana katika kulalamikia matatizo waliyonayo.

Punde askari wanawatawanya wanaogoma kwa kutumia bunduki. Bili, Diwani I na II wanamtembelea Meya. Wote wanamsifia kwa uwezo wake wa kuwatawanya wananchi. Wanne hao wanajadili jinsi ya kuuza "Fimbo ya Meya" pasi na kumhusisha Diwani III.
III
Hapa ni nyumbani kwa Meya. Dida anajizungumzia huku akifanya usafi pale. Analinganisha kazi yake ya usafi na kazi ya askari. Kwa kurejelea matukio ya  juzi ya kufurushwa kwa wafanyakazi, anaona kuwa kazi ya askari ni bora kuliko hii anayoifanya. Anasema:
Kazi ya askari nzuri
Si kama huku kufagia
Bwana anakutusi
na kukudhalilisha...

Sehemu IV
I
Afisini mwa Meya. Wawakilishi wa wafanyakazi wameleta malalamishi yao. Wao ni Tatu, Beka na Medi. Miongoni mwa wanayolalamikia ni:
  • Mishahara duni ambayo haipandishwi.
  • Kucheleweshwa kwa mishahara
  • Gharama za juu za matibabu
  • Kukithiri kwa utabaka ambapo masikini wanazidi kuwa hohehahe nao matajiri wakinufaika zaidi.
  Bela: Ni mgao wa wakubwa kula kwanza na sisi wengine kupigania makombo yanayoanguka chini. (uk70).
Kunazuka majibizano kati ya Meya na wawakilishi hao. Anaposhindwa kutatua shida zao, anawaahidi kuwa atapeleka malalamishi yao kwa madiwani. Wao wanasema kuwa wangependa kushiriki vikao hivyo. Meya anakataa hilo. Mkutano unatibuka bila maagano.
II
Ni siku moja tu baada ya Meya kukutana na wawakilishi wa wafanyakazi. Katika onyesho hili Diwani I na II wanakutana na Meya ofisini mwake. Meya ana wasiwasi kwani wafanyakazi bado wamegoma ilhali ziara ya mameya inatazamiwa kuanza alasiri. Diwani I na II wanajaribu kutoa suluhu ila hawaafikiani naye. Anajutia kutoufuata ushauri wa Diwani III.

 Gedi anaingia na habari kuwa wafanyakazi wanazidi kugoma wakiwemo wale katika uwanja wa ndege. Anasema mhazili pia amegoma na hawezi kuitwa akaja kazini kwani hakuna mafuta. Hii ni kwa sababu wafanyakazi katika bohari la mafuta wamegoma pia.

Askari I na II wanaingia na kutanguliza habari zinazompoza Meya moyo. Wanasema kuwa hakuna mgomo na tena kuwa safari ya wageni imeahirishwa. Hata hivyo, mambo yanabadilika wanaposema kuwa wametumwa kuwakamata akina Meya. Mstahiki Meya anazirai huku wenzake wakipigwa na Butwaa.  Mchezo unaishia pale. 

Marejeleo
Timothy Arege ( 2011). Mstahiki Meya. Vide-Muwa Publishers Ltd. Nairobi:Kenya

























Share this article :

Post a Comment

 
Usaidizi : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2014. Swahili - Haki zote zimehifadhiwa
Imeundwa na Creating Website Ikachapishwa na Mas Template
Imeletwa kwako na Balozihumu